HESLB na NIDA Kushirikiana Kuwatambua Waombaji Mikopo Kupitia NIN
Akiongea kwenye kikao hicho, Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB Dkt. Bill Kiwia, ameweka wazi kuwa namba ya utambulisho wa taifa itakuwa ni ya lazima katika kuomba mkopo kwa mwaka ujao wa masomo. “Tunatarajia kufungua dirisha la maombi ya mkopo mwezi Juni, 2025… kwa mwaka wa masomo wa 2025/2026 … namba ya utambulisho wa taifa itakuwa hitaji la lazima katika kujaza fomu za maombi ya mkopo, hivyo waombaji wote wanapaswa kuwa na namba hii wakati wa kujaza maombi yao ya mkopo”, amesema Dkt. Kiwia.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa NIDA, Bw. James Kaji, amesema kuwa NIDA wapo tayari kuwahudumia wanafunzi wote wanaotarajia kujiunga na vyuo vikuu na kuomba mikopo kutoka HESLB kwa kuwapatia namba za utambulisho kwa wakati na hivyo wanafunzi wanapaswa kufika kwenye ofisi za NIDA mapema ili kupatiwa namba za utambulisho. “NIDA ni maisha, kwa sasa … NIDA inaendelea kutekeleza maelekezo ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhakikisha mifumo yote ya serikali inasomana… tunawasisitiza waombaji wote wa mikopo ya elimu ya juu kuhakikisha wanafika mapema NIDA ili kupata namba ya utambulisho wa taifa”, ameeleza Bw. Kaji.